Tuesday, February 25, 2014

Waraka wa Katiba wa CCM hadharani



Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye.PICHA|MAKTABA 

NA SIA MINJA
CHANZO MWANANCHI
Waraka huo wa kurasa 22 unaoainisha mambo yenye masilahi kwa chama hicho, unawataka wajumbe wake kuutetea bungeni.
Gazeti hili limefanikiwa kuona waraka huo, ambao pamoja na mambo mengine, umetoa mapendekezo katika ibara 42 za Rasimu ya Katiba ya Tume na kupangua hoja nyingi.
Katika miongoni mwa hoja hizo, chama hicho kimesisitiza muundo wa Muungano wa Serikali mbili lakini kikapendekeza kuwapo Baraza la Wawakilishi la Tanzania Bara.
Hata hivyo, alipoulizwa kuhusu waraka huo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye aliukana akisema pamoja na msimamo wa chama hicho kuwa ni Serikali mbili, hakijafikia hatua ya kuwa na waraka.
Alisema vikao vya juu vya chama huwa havitoi waraka, bali msimamo na kwamba vyombo vingine vya chama ndivyo hutoa waraka, lakini hadi sasa havijafikia hatua hiyo.
Alisema kuwa alipoeleza maazimio ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM (NEC), alitaja msimamo wa chama hicho kuwa ni Serikali mbili zilizoboreshwa, lakini hakutaja maboresho hayo hata pale alipoulizwa na waandishi wa habari kwa sababu hayakuwa yamekamilika.
Hata hivyo, wajumbe watatu wa NEC kwa nyakati tofauti waliomba wasitajwe gazetini walisema mambo yaliyomo kwenye waraka huo ndiyo waliyokubaliana lakini hakuwa na uhakika kama ulishasambazwa.
Kwa mujibu wa waraka huo, chama hicho kinadaiwa kuainisha mambo kiliyopendekeza katika Rasimu ya Kwanza na jinsi yalivyoshughulikiwa katika Rasimu ya Pili ya Katiba.
Pia, kimeeleza mambo mengine mapya na kubainisha kasoro zake, ikiwamo utata katika mgawanyo wa majimbo ya uchaguzi.
Waraka huo pia unazungumzia sura mpya ya 17 katika Rasimu ya Katiba, ukisema inazungumzia mambo ya mpito kuelekea kupata Katiba Mpya, lakini gharama za utekelezaji wake hazitabiriki.

0 comments:

Post a Comment