Thursday, September 25, 2014



WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Dk. Abdallah Kigoda, amewataka Watanzania kuacha kununua bidhaa zisizosindikwa kwani hupunguza pato la taifa na kuchangia kupungua kwa ajira nchini.

Alisema hayo jana katika ufunguzi wa maonesho ya bidhaa kutoka China, ambazo zimetengenezwa kwa ajili ya wanunuzi wa bara la Afrika.

Alisisitiza kuwa, urafiki wa Tanzania na China unaimarika kutokana na juhudi mbali mbali zinazofanywa na serikali zote mbili hasa katika biashara.

“Tumezungumza na Serikali ya China kuona ni namna gani itaweza kutusaidia kutatua changamoto kubwa zinazotokana na uchumi, kwani wenzetu (China) wako mbele kimaendeleo zaidi yetu,” alisema Dk. Kigoda.

Akizungumzia changamoto ya kuingizwa kwa bidhaa zisizo bora kutoka uchina Dk. Kigoda, alisema serikali inashindwa kudhibiti wafanyabiashara wasio waaminifu ambao hushiriki vitendo hivyo kutokana na wingi wa mipaka inayoizunguka nchi na kukosa watendaji wa kutosha katika Shirika la Viwango Tanzania (TBS).

Aidha, Balozi wa China nchini Lu Youqing, alisema Watanzania wanakaribishwa kutangaza bidhaa nchini China katika kukuza soko la bidhaa zao.

“Kwa sasa bidhaa za Uchina zinauzwa kwa bei nafuu ili kuendana na hali ya kimaisha ya Watanzania wengi katika kusaidia upatikanaji wake bila kubagua hali ya mtu,” Alisema Balozi Youqing.

Maonyesho haya yaliyofunguliwa rasmi jijini Dar es Salaam jana, yataendelea kufanyika hadi mwishoni mwa wiki hii nia ikiwa ni kutoa fursa kwa Watanzania kufahamu bidhaa zinazozalishwa kutoka China. 




Habari na Everline bakari,

0 comments:

Post a Comment