Dar es Salaam. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amewashauri wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na CCM kuacha kuzunguka mikoani kufanya mikutano inayoeleza misimamo yao kuhusu mchakato wa Katiba Mpya kwa kuwa haina tija kwa taifa.
Ameonya kuwa mikutano hiyo inajenga mwelekeo mbaya
kwa taifa na kuhatarisha mchakato wa Katiba na kuzitaka pande hizo
kumaliza tofauti zao.
Akizungumza katika mahojiano maalumu yaliyofanyika
Dar es Salaam jana, Warioba alisema: “Kwa mustakabali mwema wa taifa,
ni muhimu makundi haya ‘ya-resolve’ (yamalize), matatizo yaliyopo kabla
ya Agosti, ili Bunge Maalumu la Katiba likirejea, wote washiriki na
kukamilisha mchakato wa kupata Katiba Mpya. Hili ni kwa masilahi ya
taifa.”
Kauli ya Waziri Mkuu huyo mstaafu ambaye pia
aliwahi kuwa Mwanasheria Mkuu, imekuja huku makundi ya Ukawa linaloundwa
na wabunge wengi wa upinzani na viongozi wa CCM wakiendelea
kung’ang’ania misimamo yao kuhusu Rasimu ya Katiba Mpya iliyowasilishwa
kwenye Bunge Maalumu la Katiba.
Wakati CCM ikipinga mapendekezo ya kuwapo kwa mfumo wa serikali tatu uliomo kwenye Rasimu, Ukawa unaunga mkono mapendekezo hayo.
Aprili 16, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim
Lipumba aliiongoza Ukawa kutoka ndani ya Bunge la Katiba baada ya
kumaliza kuchangia mjadala huo, kwa madai ya kutokutendewa haki na CCM
katika mambo mbalimbali ikiwamo kupinga mapendekezo ya upinzani hata
yale ya msingi akisema hawawezi kuwa sehemu ya watu wanaosambaza chuki
na kuwa sehemu ya kuibomoa nchi.
Siku chache baadaye, Ukawa ulianza mikutano nchi
nzima kwa kile ulichodai kuwaeleza wananchi namna CCM inavyotaka
kuchakachua maoni yao yaliyokusanywa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Kwa upande wake, CCM imekuwa ikifanya mikutano kueleza msimamo na sababu za kutaka kuendelea kwa muundo wa serikali mbili.
Jaji Warioba alisema makundi hayo yana nafasi ya
kumaliza tofauti zao kabla ya Bunge Maalumu la Katiba kuanza tena vikao
vyake, hivyo kuliwezesha taifa kupata Katiba Mpya.
Alisema makundi hayo yasipopatana yanaweza kuhatarisha mustakabali wa taifa hata amani iliyopo.
Alionya kuwa amani iliyopo nchini ikivurugika kwa sababu yoyote ni vigumu kuirejesha na kwamba watakaotaabika ni wananchi.
Jaji Warioba ambaye aliwahi kuongoza Tume ya
Rushwa iliyoundwa na Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, alisema
amani ya Tanzania ikivurugika kutokana na makundi kupingana katika
mchakato wa Katiba wanasiasa ndio watakaonyooshewa vidole.
credit: Mwananchi
Augustina kawau.
credit: Mwananchi
Augustina kawau.
0 comments:
Post a Comment